A blog that gives out financial institutions news on time with accurate informations.


Sunday, April 3, 2022

WAKAZI WA RUANGWA WAASWA KUSHIRIKI KIKAMILIFU ZOEZI LA SENSA YA WATU NA MAKAZI


Na Mwandishi wetu, Ruangwa

Tanzania itafanya Sensa ya Watu na Makazi mwezi Agosti mwaka 2022 katika siku itakayotangazwa na Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hayo yametanabaishwa na Mratibu wa Sensa ya Watu na Makazi Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, Mchumi-Tumsime Lazaro Mutta kwenye mahojiano maalumu na mwandishi wetu katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya ya Ruangwa, mkoani Lindi.

Mchumi-Tumsime amesema "Kabla ya zoezi la kuhesabu watu wote watakaolala ndani ya mipaka ya nchi usiku wa kuamkia Siku ya Sensa, shughuli mbalimbali za maandalizi hufanyika ambazo hujumuisha utoaji elimu kwa lengo la kuuelimisha umma juu ya umuhimu wa Sensa ili kuhakikisha kila mmoja anatambua umuhimu wa kuhesabiwa na kuhamasika kuhakikisha kwamba anahesabiwa na anahesabiwa mara moja tu."

Aidha, Mchumi-Lazaro Muta ametumia fursa hiyo kuieleza jamii kuhusu lengo la Sensa ya Watu na Makazi, "Lengo la Sensa ya Watu na Makazi ni kupata taarifa sahihi za kidemografia, kijamii, kiuchumi na hali ya mazingira kwa lengo la kupata takwimu sahihi zitakazoiwezesha Serikali na wadau wengine kupanga kwa usahihi mipango ya maendeleo ya watu wake katika sekta mbalimbali za elimu, afya, hali ya ajira, miundombinu kama barabara, nishati na maji safi".

Ikumbukwe Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Kassim Majaliwa katika moja hotuba zake kwa wadau wa Sensa ya Watu na Makazi amewataka viongozi wa Mikoa, Wilaya na Kata kuhakikisha wanaongeza kasi katika uratibu wa maandalizi ya zoezi hili.

"Zoezi hili linatakiwa kutekelezwa kwa operesheni na kwa kipindi maalum kama ilivyokuwa katika miradi iliyojengwa kupitia fedha za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19," alisema Mhe.Majaliwa.

Awali, Mchumi-Lazaro Mutta amewaasa wakazi wa Ruangwa kushiriki ipasavyo zoezi hilo "Wakati wa Sensa ya Watu na Makazi tunachotakiwa kufanya ni kumpa ushirikiano wa kutosha Karani wa Sensa atakapotembelea katika kaya kwa kujibu maswali yote atakayouliza kwa usahihi".
Share:

0 comments:

Post a Comment


Propellerads

Search Brazuka Kibenki

FOLLOW US ON FACEBOOK

  • ()
  • ()
Show more

Labels

Blog Archive