A blog that gives out financial institutions news on time with accurate informations.


Monday, May 10, 2021

BENKI YA NBC YAZINDUA KLABU YA WAFANYABIASHARA MKOANI KIGOMA

Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma Rashid Mchatta (wapili kushoto), pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Theobald Sabi wakifurahia baada ya kufanya uzinduzi rasmi wa NBC Biashara Club kwa Mkoa wa Kigoma uliofanyika katika Hoteli ya Lake Tanganyika wenye lengo la kuwakutanisha wateja wake wafanya biashara na wenye viwanda na wadau wengine. Wengine pichani kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Wafanayabiashara Wadogo na wa Kati wa benki ya NBC, Mussa Mwinyidaho pamojana Mteja wa Benki hiyo, Marietha Patrick.
Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma, Rashid Mchatta (wa sita kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi (wa saba kushoto) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa wa Kigoma baada ya uzinduzi rasmi wa NBC Biashara Club kwa Mkoa huo uliofanyika katika Hoteli ya Lake Tanganyika mjini Kigoma.

Benki ya NBC imezindua klabu ya wafanyabiashara wa benki hiyo mkoani Kigoma ikiwa ni sehemu ya mipango ya benki hiyo kusogeza huduma kwa wateja wake sambamba na kujenga mtandao ambao utawasaidia wafanyabiashara wateja wa benki hiyo kufanya biashara zao kwa tija.

Theobald Sabi ni Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC,Theobald Sabi akizungumza kwenye uzinduzi wa klabu hiyo ya wafanyabiashara kwa mkoa Kigoma alisema kuwa lengo kubwa la klabu hiyo kuwakutanisha pamoja wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali kwenye sekta ya biashara kuzungumza kwa pamoja changamoto zinazowakabili wafanyabiashara hao na kuzitatua.

Kwenye business club pia tuna Business Clinic ambapo wateja licha ya kukutana wao kwa wao kujenga mtandao wa kubadilishana taarifa na uzoefu wa biashara pia watakutana na wataalam kutoka sekta mbalimbali kama TCCIA, SIDO, BRELA, TRA, kampuni ya maswala ya ukaguzi wa fedha Delloitte na wadau wengine ambao watawasaidia kujua taratibu mbalimbali za kufanya biashara,” Alisema Sabi Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa klabu za wafanyabiashara pia zinawajenga wafanyabiashara na kuwapa uelewa wa namna ya kushiriki kwenye maonyesho mbalimbali kwa ajili ya kutangaza bidhaa zao na kufungua masoko ambapo biashara za kuvuka mpaka zimekuwa zikiangaliwa pia kupitia klabu hizo.

Alisema kuwa kupitia kwenye klabu za biashara benki hiyo imekuwa ikitoa mafunzo kwa wafanyabiashara hao ambao ndiyo msingi mkubwa wa kuwafanya wafanye biashara zao kwa tija ambapo mafunzo yanayotolewa yanazingatia taratibu mbalimbali za kuwafanya wapige hatua za maendeleo kwennye kusimamia biashara.

Kuna watu wanafanya biashara hawana elimu ya usimamizi wa biashara (Business Management) hivyo kwa semina hizo tunawapa uelewa wa jambo hilo, mbinu za kutafuta masoko, mbinu za kujenga mtandao lakini pia tunawapa uelewa wa namba ya kuandika michanganuo ya biashara kwa ajili ya kuomba mikopo taasisi za fedha na kuwafanya waweze kumiliki mawazo yaliyopo kwenye michanganuo hiyo na kuifanyia kazi kwa faida,”Alisema.

Mkurugenzi huyo wa NBC alisema kuwa kubwa ambalo ndilo msingi wa kuanzishwa kwa klabu za wafanyabiashara ni kuwafanya wafanye biashara zao kwa faida na kukua kibiashara ambako kutaongeza mapato yao lakini pia kutaongeza mapato ya serikali na mwisho wa siku wafanyabiashara hao watakuwa na uwezo wa kukopa mikopo mikubwa na kurejesha jambo ambalo ndiyo msingi mkuu wa benki katika kujiendesha kwa faida.

Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma, Nd Rashid Mchatta akizindua klabu ya biashara kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Nd Thobias Andengenye alisema kuwa mafunzo na kujenga mtandao kwa wafanyabiashara ndiyo msingi mkubwa utakaowawezesha wafanyabiashara kufanya biashara zao kwa faida.

Katika hotuba yake, Nd Mchatta alisema kuwa biashara ambazo zinaendeshwa kwa kufuata maelekezo ya watalaam zimekuwa zikifanyika kwa mafanikio na hata kunapotokea changamoto inakuwa rahisi kukabili changamoto hiyo.

Alisema kuwa kuwepo kwa vikao vya wafanyabiashara wao kwa wao, wao na wadau wengine na wao na serikali kuna faida kubwa katika kuifanya sekta ya biashara kuwa na tija lakini pia inasaidia kukabili changamoto ambazo zimekuwa zikilalamikiwa na kila upande kwenye biashara.

Tukikaa kwa pamoja na kujadili mambo yanayohusu biashara tutazipatia utatuzi changamoto zinazojitokeza maana wafanyabiashara wana malalamiko yao kwa taasisi za serikali zinazosimamia biashara na serikali nayo inalalamika kwa ukwepaji kodi, bidhaa duni na vitu vingine hivyo klabu za biashara zinatufanya kukutana pamoja na kuzungumza tofauti zetu,” Alisema Mkuu wa mkoa Kigoma.

Uzinduzi wa klabu ya wafanyabiashara mkoa wa Kigoma ulitanguliwa na semina kwa wafanyabiashara wa mjini Kigoma ambapo mada mbalimbali zilitolewa kuwezesha wafanyabiashara kuwa na uelewa wa mambo mbalimbali ya biashara.

Baadhi ya wafanyabiashara walioshiriki kwenye semina na uzinduzi wa klabu ya wafnyabiashara wameeleza faida kubwa ambayo wameipata kwa kuhudhuria semina kutokana na mada zilizotolewa kuishi ndani ya wafanyabiashara ambazo zitawafanya kufanya biashara zao kwa faida.

Kilahumba Kivumo ambaye ni mfanyabiashara mkoni humo akizungumza wakati wa uzinduzi wa klabu ya wafanyabiashara wa mkoa Kigoma, alisema kuwa klabu hiyo ni wazo zuri la litawasaidia kupata mahali pa kuzungumza changamoto zao na namna ya kuzitafutia ufumbuzi.

Alisema kuwa changamoto kwenye biashara ni nyingi ikiwemo taratibu za kupata mikopo ambapo bado taarifa zake hazijawa wazi kwa wafanyabiashara lakini pia vikwazo katika biashara za kuvuka mpaka na vizuizi mbalimbali njiani ambavyo vinawakatisha tama wafanyabiashara hivyo Benki ya NBC imeingia Kigoma kwa wakati muafaka na imeleta matumaini mapya katika biashara zao.
Share:

0 comments:

Post a Comment


Propellerads

Search Brazuka Kibenki

FOLLOW US ON FACEBOOK

  • ()
  • ()
Show more

Labels

Blog Archive