A blog that gives out financial institutions news on time with accurate informations.


Sunday, October 18, 2020

Benki Ya CRDB Yazindua Kampeni Ya "Jipe Tano" Kuhamasisha Utamaduni Wa Kujiwekea Akiba Kwa Wateja

Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi, Benki ya CRDB, Stephen Adili akizungumza na Waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa kampeni ya "Jipe Tano" inayolenga kuhamasisha wateja kujenga utamaduni wa kujiwekea akiba. Benki ya CRDB imetenga Shilingi milioni 100 kama zawadi kwa wateja ambao watakuwa wakiweka akiba mara kwa mara katika akaunti zao, ambapo wateja 240 watakuwa wakijishindia fedha kila siku.

Benki ya CRDB imezindua kampeni maalum ya kuhamasisha wateja na Watanzania kwa ujumla kujenga utamaduni wa kujiwekea akiba iliyopewa jina la “Jipe Tano”. Akizungumza katika uzinduzi huo Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi Benki ya CRDB, Stephen Adili amesema kampeni hiyo inalenga kuwasaidia wateja kufikia malengo yao ya kimaisha pamoja na kumudu gharama mbalimbali za maisha kupitia utamaduni wa kujiwekea akiba.

Tunatambua wateja wetu wana malengo ambayo wamejiwekea katika maisha yao, na sisi kama Benki ya kizalendo tuna jukumu la kuhakikisha wateja wetu wanafikia malengo yao kupitia huduma na bidhaa bunifu zinazotolewa na Benki yetu ikiwemo huduma ya kuweka akiba kupitia akaunti mbalimbali,” alisema Adili.

Adili alisema kampeni hiyo ya katika kampeni hiyo ya “Jipe Tano”, Benki ya CRDB imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 ambapo wateja watakuwa wakijishindia zawadi ya shilingi elfu tano kila watakapokuwa wakiweka akiba katika akaunti zao ikiwamo akaunti ya Watoto Junior Jumbo, Akaunti ya Malkia kwa ajili ya wanawake, Akaunti ya Scholar kwa ajili ya wanafunzi, Akaunti ya Tanzanite kwa ajili ya Watanzania waishio nje ya nchi, akaunti ya pensheni kwa ajili ya wastaasfu, Akaunti ya FahariKilimo kwa ajili ya wakulima na akaunti nyengine za uwekezaji kama Thamani, Dhahabu na akaunti za muda maalum.

Kila mteja atakapokuwa akiweka akiba kwenye akaunti yake atakuwa anapata nafasi ya kujishindia shilingi elfu tano kila siku, tunafanya hivi ili kuongeza hamasa kwa wateja kuweka akiba zaidi na kujenga utamaduni huu kwa watanzania,” aliongezea Adili huku akibainisha Benki hiyo itakuwa ikitoa zawadi kwa washindi 240 kila siku hadi mwishoni mwa mwezi Desemba kampeni hiyo itakapofikia kilele.

Mkuu wa Kitengo cha Masoko Benki ya CRDB, Joseline Kamuhanda akizungumza na Waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa kampeni ya "Jipe Tano" inayolenga kuhamasisha wateja kujenga utamaduni wa kujiwekea akiba. Benki ya CRDB imetenga Shilingi milioni 100 kama zawadi kwa wateja ambao watakuwa wakiweka akiba mara kwa mara katika akaunti zao, ambapo wateja 240 watakuwa wakijishindia fedha kila siku.

Akielezea namna ambavyo wateja watakuwa wakijishindia katika kampeni hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Masoko Benki ya CRDB, Joseline Kamuhanda alisema wateja watahitajika kuweka akiba kwenye akaunti zao mara kwa mara ili kushinda zaidi, huku akiwahamasisha wale ambao bado hawana akaunti Benki ya CRDB kufungua na kuanza kujiwekea akiba.

Kila unapoweka akiba kwenye akaunti yako yoyote iwe kwenye tawi, CRDB Wakala au kupokea salio kupitia SimBanking, Internet banking au kutoka mitandao ya simu na taasisi nyengine za fedha kuingia akaunti yako ya Benki ya CRDB, unajiwekea nafasi ya kushinda shilingi elfu tano kila mara, na ndiomana tunasema Jipe Tano,” alisisitiza Kamuhanda.

Kamuhanda alisema Benki ya CRDB imeendelea kuboresha huduma na miundombinu yake ya kutoa huduma hususan ile ya kidijitali, ambapo aliwataka wateja kutumia huduma za CRDB Wakala, SimBanking na Internet banking kufanya miamala yao ya kifedha, huku akiwataka wateja pia kuhamasishana kutumia akaunti za benki kupokea malipo na kuweka akiba.


Ukitaka kumlipa mtu muulize kwanza una akaunti Benki ya CRDB akisema hana mwambie afungue ili wakati unamtumia na yeye apate tano, wanasema vizuri kula na nduguyo,” aliongezea Kamuhanda.

Kampeni hii ya Jipe Tano nimuendelezo wa jitihada za Benki ya CRDB katika kutoa elimu ya huduma za fedha kwa Watanzania, ambapo mapema mwaka huu Benki hiyo iliendesha kampeni ya Popote Inatiki ikihamasisha wateja kutumia mifumo ya kidijitali kupata huduma kwa urahisi na usalama.
Share:

0 comments:

Post a Comment


Propellerads

Search Brazuka Kibenki

FOLLOW US ON FACEBOOK

  • ()
  • ()
Show more

Labels

Blog Archive