A blog that gives out financial institutions news on time with accurate informations.


Sunday, August 27, 2023

Rais wa Zanzibar aipongeza Benki ya Absa Tanzania kusaidia juhudi za kupunguza na kuepusha vifo vya mama wajawazito na watoto.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk Hussein Ali Mwinyi (katikati), akishiriki matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon 2023 mjini Zanzibar jana zilizofanyika kwa udhamini mkuu wa Benki ya Absa Tanzania. Wengine kutoka kushoto ni, Mke wa Rais, mama Mariam Mwinyi, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa, Obedi Laiser, Naibu Waziri wa Wizara ya Afya Zanzibar, Mhe. Hassan Khamis Hafidh na Mkurugenzi wa Shirika la Amref, Dk. Florence Temu. Hafla hiyo ilikuwa na lengo la kuchangisha fedha kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba kwa uzazi salama na afya ya mama na mtoto.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk Hussein Ali Mwinyi (wa pili kushoto), akipata maelekezo kuhusu huduma za kibenki za Benki ya Absa, kutoka Kwa Meneja Mahusiano wa Wateja Maalumu wa benki hiyo, Salim Khamis Salum wakati akiwasili katika viwanja vya Maisara mara baada ya kushiriki matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon 2023 zilizofanyika kwa udhamini wa Benki ya Absa, mjini Zanzibar jana. Kushoto kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa, Obedi Laiser. Hafla hiyo ilikuwa na lengo la kuchangisha fedha kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba kwa uzazi salama na afya ya mama na mtoto.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk Hussein Ali Mwinyi (kushoto), akizungumza katika hafla ya matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon 2023 zilizofanyika Kwa udhamini wa Benki ya Absa mjini Zanzibar jana. Hafla hiyo ilikuwa na lengo la kuchangisha fedha kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba kwa uzazi salama na afya ya mama na mtoto.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Obedi Laiser (kulia), akitoa hotuba yake katika hafla ya matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon zilizofanyika Kwa udhamini wa Benki ya Absa mjini Zanzibar jana. Mgeni rasmi alikuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi (kushoto). Hafla hiyo ilikuwa na lengo la kuchangisha fedha kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba kwa uzazi salama na afya ya mama na mtoto.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk. Hussein Ali Mwinyi (wa nne kushoto) akikabidhi cheti cha shukurani Kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Obedi Laiser, Kwa kutambua udhamini mkuu wa Benki hiyo katika mbio fupi na matembezi ya Amref Wogging Marathon zilizofanyika visiwani Zanzibar jana. Hafla hiyo ilikuwa na lengo la kuchangisha fedha kusaidia upatikanaji wa vifaa tiba kwa uzazi salama na afya ya mama na mtoto.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi (wa tatu kushoto), akikataa utepe kuashiria makabidhiano rasmi ya gari la kliniki inayotembea lilolilotokewa na Shirika la Amref kwenda Wizara ya Afya ya visiwani humo. Ilikuwa ni wakati wa hitimisho la matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon zilizofanyika mjini Zanzibar chini ya udhamini mkuu wa Benki ya Absa Tanzania.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi (wa nne kushoto), viongozi kutoka jukwaa kuu, wakipozi Kwa picha ya kumbukumbu pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa Benki ya Absa, wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wao, Obedi Laiser muda mfupi baada ya kukamilika kwa matembezi na mbio fupi za Amref Wogging Marathon zilizofanyika mjini Zanzibar jana chini ya udhamini mkuu wa benki hiyo.

Na mwandishi wetu, Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk Hussein Ali Mwinyi ameipongeza Benki ya Absa Tanzania, kwa kudhamini matembezi na mbio fupi zenye lengo la kuchangia vifaa tiba kwa uzazi salama wa mama na mtoto.

Akizungumza mara baada ya matembezi hayo yaliyoitwa ‘Wogging Marathon 2023’ yaliyoandaliwa na Shirika la Amref Health Afrika kwa kushirikiana na Serikali ya Zanzibar chini ya udhamini wa Absa katika Viwanja vya Maisara, mjini Zanzibar jana, Rais Mwinyi alisema anatambua na kuthamini udhamini mkubwa wa Benki ya Absa pamoja na waandaaji wa matembezi hayo.

Kwa niaba ya serikali natoa shukurani kwa Benki ya Absa Tanzania na kuwataka waendelee kutupa ushirikiano katika kuhakikisha tunafanikiwa katika malengo yetu ya kupunguza idadi ya vifo vya mama wajawazito na watoto vinavyotokana na uzazi".

Nimefurahi kusikia kuwa kampeni hii ni ya miaka mitatu na ilianza tokea mwaka jana ikiwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni moja huku taarifa nilizonazo zikionyesha kuwa hadi sasa ahadi za jumla ya shs milioni 792 zimetolewa huku kilichopatikana ni shs milioni 557”, alisema mheshimiwa rais.

Akizungumza mara baada ya matembezi hayo yaliyokuwa ya umbali wa kilomita tano na kumi, ambapo pia alishiriki matembezi hayo akiwa na mkewe Mama Mariam Mwinyi, viongozi kisiasa, kiserikali, taasisi za umma na binafsi na wananchi ndani ya kisiwa hicho na wageni wengine kutoka nje ya Zanzibar alisema, kampeni ya Uzazi Salama inaunga mkono juhudi za serikali katika kupunguza na kuepusha vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga kutokana na ukweli kuwa bado takwimu za vifo hivyo bado vipo juu.

Takwimu zinaonyesha vifo vya kina mama 134 kati ya vizazi hai 100 kwa mwaka na vifo 28 vya watoto wachanga kati ya vizazi hai 1,000 kwa mujibu wa takwimu za Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria Tanzania (TDHS) za mwaka 2017”, alisema Rais Mwinyi akiongeza kuwa kiwango hicho kinasababishwa na changamoto mbalimbali zikiwemo upungufu wa vifaa tiba, uhaba wa wahudumu pamoja na kukosekana kwa dawa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa, Bwana Obedi Laiser alisema kampeni hii inaenda sambamba na dhumuni kuu la benki ya Absa ambalo ni kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, mtu mmoja baada ya mwengine katika kuiwezesha jamii yenye afya bora na mustakabali mzuri.

Sisi kama Absa tunatambua juhudi kubwa zinazofanywa na serikali ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya pamoja na mashirika kama Amref katika kuleta mabadiliko katika jamii hususani katika suala zima la afya ya mama wajawazito na mtoto kwani afya ya mtoto ni msingi wa Taifa la watu wa sasa na wa kesho".

Tutaendelea kushirikiana na serikali za Zanzibar katika jitihada zake za kuwaletea wananchi wake maendeleo, tuna malengo makubwa ya kibiashara hapa Zanzibar katika kutanua huduma zetu za kibenki, na tutaendelea pia kushirikiana na Amref katika jitihada hizi za kuokoa maisha ya mama na mtoto japo hii ni mara yetu ya kwanza”, alisema Bwana Laiser.

Matembezi na mbio fupi za Amref wogging ni hafla la kila mwaka inayoandaliwa na shirika hilo kwa ushirikiano na serikali huku yakiwezeshwa kwa udhamini wa taasisi mbalimbali, wananchi pamoja na wadau wengine yakiwa na lengo kutafutu suluhu za changamoto zinazosababisha vifo vya wamama wajawazito na watoto wachanga nchini.
Share:

0 comments:

Post a Comment


Propellerads

Search Brazuka Kibenki

FOLLOW US ON FACEBOOK

  • ()
  • ()
Show more

Labels

Blog Archive